KIWANDA CHA CHUMVI UVINZA CHATAKIWA KUONGEZA UZALISHAJI

 Na Mwajabu Hoza, Kigoma

KATIBU mkuu wizara ya viwanda na biashara Prof. Riziki Shemdoe amemtaka mwekezaji wa  kiwanda cha chumvi cha Nyanza Mines kilichopo wilaya ya Uvinza mkoa wa Kigoma kuongeza uzalishaji pamoja na kupanua wigo wa soko la ndani ili serikali iweze kunufaika na uwekezaji huo.

Prof. Riziki Shemdoe alisema hayo mara baada ya kutembelea kiwanda hicho na kujionea shughuli za uzalishaji ambapo amesema lengo la ziara yake ni kutekeleza maagizo ya Raisi wa Jamuhuri ya Mungano wa Tanzania Mhe. John Pombe Magufuli aliyoyatoa wakati wa kampeni zake katika wilaya hiyo.

Alisema uwekezaji unaofanyika katika kiwanda hicho ni mkubwa na soko kubwa likiwa nchi Jirani ya Congo DRC na Burundi kwa asilimia 60 na asilimia 40 ikiwa ni soko la ndani ni lazima serikali inufaike na uwekezaji huo huku akiitaka halmashauri kukaa pamoja na kufikia muafaka wa utoaji wa tozo zilizopo kisheria.

“Kwa sasa kiwanda hiki kinazalisha tani elfu 20 hadi 25 lakini lengo lilikuwa ni uzalishaji wa tani elfu 50 ambayo haijafikiwa kutokana na changamoto ya mafuriko kutoka katika mto malagalasi na kusababisha shughuli za uzalishaji kusimama” aliongeza Prof. Shemdoe.

Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara Prof. Riziki Shemdoe akizungumza na waandishi wa habari wakati akikagua kiwanda cha Chumvi Uvinza. (Picha Zote Na Mwajabu Kigaza) 

Weja Ng’olo ambaye ni mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Uvinza alieleza kutokuwepo kwa ushirikiano baina ya halmashauri na kiwanda na hilo linachangiwa na kutokuwepo kwa uwazi wa kiasi kinachokusanywa ambapo hali hiyo inachangia kurudisha nyuma shighuli za maendeleo.

“ Tozo zilizopo zipo kisheria wanatakiwa kuilipa halmashauri kiasi cha 0.3 ya ushuru wa huduma lakini pia ushiriki wa miradi ya maendeleo kwenye jamii umekuwa ni mdogo mpaka kusukumwa na kwa mwaka wanalipa kiasi kisichozidi milioni 10 , ninachoshauri tu wawe wawazi na walipe tozo zoto ambazo zipo kisheria” alisema Weja.

Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na biashara Prof. Riziki Shemdoe akiwa na  meneja wa kiwanda cha chumvi Uvinza Boniphace Mwaipopo wakati akikagua kiwanda hicho.

Emmanuel Miselya kutoka mamlaka ya maendeleo ya biashara Tanzania Tan tred akaeleza namna ambavyo watahakikisha upatikanaji wa  masoko ya ndani na nje ya nchi unaongezeka lakini pia ameeleza sambamba na hilo watahakikisha wanatoa ushauri kwa kiwanda hicho kuhakikisha soko linakuwa zaidi.

Aidha meneja wa kiwanda hicho Boniphace Mwaipopo ameeleza licha ya kutoa ajira ya zaidi ya 500 kwa jamii inayozunguka wilaya ya Uvinza lakini bado kuna changamoto kubwa ya uharibifu wa miundombinu ya kiwanda hicho jambo linalochangia kusimama kwa shughuli za uzalishaji kwa muda ili kupata vifaa vipya ambavyo vimekuwa vikiharibiwa na jamii inayozunguka kkiwanda hicho.

Idd Kimondo ni miongoni mwa vibarua ambapo ameeleza kuwa kiwanda hicho kimekuwa msaada mkubwa kwao katika kukuza uchumi wao kwenye familia lakini pia kujiepusha na vitendo vibaya mtaani ikiwemo wizi na uvutaji wa bangi huku baadhi ya kinamama nao wakipata fedha za kusomesha watoto wao.

Baadhi ya vibarua katika kiwanda cha chumvi Uvinza wakiendelea na shughuri.


 

 

Post a Comment

0 Comments