WATUMISHI TAMISEMI NA MANISPAA YA KIGOMA UJIJI WAPANDISHWA KIZIMBANI KWA UHUJUMU UCHUMI

Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya Igunga Athuman Msabila (anayeongea na simu) akiwa kwenye gari la polisi akipelekwa gereza la Bangwe mjini Kigoma baada ya yeye na wenzake 10 kusomewa mashitaka 11 ikiwemo la uhujumu uchumi.



Na Mwandishi Wetu, Kigoma
KESI ya Uhujumu uchumi namba 3 ya mwaka 2023 yenye mashtaka 11 ikiwemo kosa la utakatishaji fedha kiasi cha Tsh 463.5 milioni inayowahusu watumishi 11 wa Manispaa ya Kigoma Ujiji na Tamisemi.

Akisoma mashtaka hayo mbele ya hakimu Mfawidhi wa mahakama hiyo Hassan Momba, Wakili mwandamizi wa
serikali Anosisye Erasto ameieleza mahakama kuwa washitakiwa walitenda makosa hayo kati ya juni 1, 2022 na Juni 5, 2023 katika Manispaa ya Kigoma ujiji na Jiji la Dodoma.

Baadhi ya mashitaka wanayoshitakiwa ni pamoja na kula njama kwa nia ya kutenda kosa, kugushi, matumizi mabaya ya madaraka, kutakatisha fedha, kuisababishia mamlaka ya serikali hasara.

Washitakiwa katika kesi hiyo ni pamoja na aliyekuwa mkurugenzi wa Manispaa ya Kigoma ujiji Athumani Msabila, watumishi wa ofisi ya Tawala za Mikoa na serikali za Mitaa(Tamisemi) Dodoma Aidan Mponzi na Tumsifu Kachira.

Wengine ni Watumishi toka ofisi ya Manispaa ya Kigoma Ujiji Frednand Filimbi, Salum Juma, Moses Zahuye, Joel Shirima, Jema Mbilinyi, Kombe Kabichi, Frank Nguvumali na Bayaga Ntamasambilo kutoka ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kigoma.

Katika kesi hiyo washitakiwa wanasimamiwa na mawakili wanne ambao ni Sadiki Aliki, Michael Mwangati, Eliutha Kvyiro na Victoria Nyembea.

Aidha washtakiwa hao hawakutakiwa kujibu chochote kutona na mahakama kutokuwa na mamlaka ya kusikiliza mashauri yao ikiwemo shitaka la uhujumu uchumi na kuisababishia serikali hasara.

Kesi hiyo imehairishwa hadi novemba 20 mwaka huu itakapotajwa tena kwaajili ya kutoa uamuzi wa dhamana kwa washitakiwa watano ambao hawahusiki na shitaka la utakatishaji fedha kama watakuwa na haki ya kupata dhamana.

Post a Comment

0 Comments