Na Mwandishi Wetu Lushoto
MJUMBE wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu
ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa amewataka wakulima wa
chai wilayani Lushoto wajiandae na kilimo hicho kwa kuwa kiwanda cha chai cha
Mponde kilichopo katika jimbo la Bumbuli
kinatarajiwa kuanza uzalishaji hivi karibuni baada ya kusimama kwa muda mrefu.
Kiwanda
cha chai Mponde ni miongoni mwa viwanda vya kusindika majani mabichi ya chai
katika Halmashauri ya Bumbuli na hutegemewa na wakulima wadogo wa chai wapatao
5,000 kama soko la majani mabichi ya chai kutoka katika mashamba yao, ambapo
uzalishaji ulisimama kufuatia mgogoro uliojitokeza mwaka 2013.
Mheshimiwa Majaliwa alitoa kauli hiyo jana jioni (Ijumaa, Oktoba 9, 2020) alipozungumza na wananchi wa jimbo la Bumbuli wilayani Lushoto, Tanga katika mkutano wa kampeni uliofanyika Kata ya Soni wakati alipomuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM Rais Dkt. John Pombe Magufuli na wagombea udiwani baada ya mgombea ubunge wa jimbo hilo January Makamba kupita bila ya kupingwa.
“Najua
msimu huu mmehangaika sana, lazima kiwanda chetu kianze kazi na hatua zote za
msingi zimeshakamilika. Msimamizi mkuu ni Msajili wa Hazina na mwekezaji ni mifuko ya hifadhi ya jamiii ya PSSSF na WCF, ambao
walishakuja kufanya ukaguzi ila kuna mitambo inahitaji vipuri na tumeagiza
vichongwe ili kazi ianze chai isindikwe.”
Alisema mitambo ile ni ya miaka
mingi sana na hata teknolojia yake
imepitwa na wakati, hivyo kwa sasa wameagiza vipuri vichongwe ili chai ya
wakulima iendelee kusindikwa wakati wawekezaji hao wakitafuta mashine nyingine
mpya na za kisasa ambazo zitakapopatikana zitabadilishwa huku zoezi la
usindikaji likiwa linaendelea.
Mheshimiwa Majaliwa alisema mpango
wa kibiashara (Business Plan) wa kukarabati kiwanda hicho uliandaliwa na
umeshawasilishwa Wizara ya Fedha na Mipango kama sehemu ya matakwa ya wizara
ili kuridhia matumizi ya fedha kutoka kwenye mifuko hiyo kiasi cha shilingi
bilioni 4.05 kwa ajili ya ukarabati na uendeshaji wa kiwanda.
0 Comments