Na Mwandishi Wetu – Dar es Salaam
Upasuaji wa kisasa wa kuondoa uvimbe wa saratani pasipo kuondoa
titi lote lililoathirika umeleta ahueni kwa wagonjwa na kupunguza unyanyapaa kwa
wanawake nchini.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI), Dkt.
Julius Mwaiselage alieleza hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari
katika mahojiano maalum, kuhusu mwezi Oktoba ambao ni maalum Kidunia kwa ajili
ya uelimishaji, uhamasishaji, uchunguzi na matibabu ya saratani hiyo.
Alisema wastani wa wanawake 100 wanaogundulika na saratani hiyo
ikiwa katika hatua za awali, huondolewa uvimbe kwa njia ya upasuaji pasipo
kung’olewa titi lote lililoathiriwa kila mwaka ambapo huduma hiyo ilianza
kutolewa rasmi mwaka 2016 nchini na wataalamu wa ORCI wakishirikiana na wenzao
wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH- Mloganzila).
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) Dk. Julius Mwaiselage akizungumza.
“Zamani kwa kuwa hatukuwa na mashine za kisasa za tiba mionzi,
matibabu yalikuwa ni lazima kuondoa titi lote, changamoto nyingine tuliyokuwa
tunakabiliana nayo ni wagonjwa hawa kuchelewa kuja hospitalini, wanakuja
ugonjwa ukiwa umefikia hatua za juu mno, haikuwa rahisi kupata matokeo mazuri
ya tiba.
“Lakini kutokana na maboresho yaliyofanywa na Serikali kwa
kutumia mashine hii ya ‘Linear accelerator’, tunao uwezo wa kuchunguza na
kutibu kwa kuondoa ule uvimbe tu na kuliacha titi, baada ya upasuaji huo
mgonjwa anaendelea na matibabu ya mionzi kupitia mashine ya kisasa tuliyonayo
hapa ORCI,” amesisitiza.
Aidha alisema kuwa kwa wale waliofanyiwa upasuaji na kuondolewa titi
lote jitihada zinafanyika ambapo tayari wataalamu wapo nchini China wakijifunza
jinsi ya kufanya upasuaji wa kupandikiza matiti.
Amesema Shirika la Afya Duniani (WHO) linakadiria kila mwaka
Tanzania kuna wagonjwa wapya 42,000 wa saratani aina zote, saratani ya matiti
inaongoza duniani kote kwa kuathiri wanawake kwa asilimia 99, wanaume asilimia
moja huku takwimu hiyo ikiongezeka kwa kasi.
0 Comments