MADIWANI MANISPAA YA KIGOMA UJIJI WATAKIWA KUSIMAMIA MAPATO

 


Na Mwajabu Hoza

MKURUGENZI wa Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji Mwailwa Pangani amewataka madiwani wote waliokabidhiwa hati ya kuchaguliwa kuwa madiwani katika uchaguzi mkuu uliofanyika octoba 28 ya mwaka huu kuhakikisha wanasimamia vyema ukusanyaji wa mapato ya halmashauri hiyo kutoka katika vyanzo vilivyopo kwenye kata zao pamoja na kubuni vyanzo vipya vya mapato.

Akizungumza mara baada ya kukabidhi hati hizo kwa madiwani wapatao 19 Mwailwa Pangani amesema ili halmashauri hiyo iweze kusonga mbele katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ni lazima madiwani wawajibike ipasavyo katika suala zima la ukusanyaji wa mapato lakini pia kusimamia vyema miradi ya maendeleo kwenye maeneo yao.

“ Baraza la madiwani lililopita madiwani wengi walikuwa wakidai stahiki zao na hilo linatokana na kusuasua kwa ukusanyaji wa mapato hivyo baraza hili kwa kuwa wote ni wamoja na wanasimamia ilani ya chama chao ni wazi kuwa watakusanya mapato na wasitegemee kuwa manispaa kuna hela wanakuja kunufaika hapana bali wao wanatakiwa kuiletea halmshauri hela kutoka katika vyanzo walivyonavyo” amesema



Baadhi ya madiwani hao wameeleza ambavyo watawajibika kusimamia vyema utekelezaji wa ilani ya chama cha Mapinduzi CCM kupitia vipaumbele ambavyo wameviainisha ili  kuhakikisha wanatekeleza miradi yote kwa ufanisi sanjari  na wanaondoa tatizo la upatikanaji wa hati chafu kwa halmashauri hiyo.

Sharon Mashanya , Abdallah Kiyembe na Mussa Maulidi kwa nyakati tofauti wamesema vipaimbele vyao vya kwanza  ni pamoja na miundombinu ya barabara na madaraja, vifaa kwa ajili ya sekta ya afya, kufufua masoko pamoja na kuongeza mitaji kwa vijana, wanawake na walemavu sanjari na kushawishi uwekezaji ndani ya manispaa hiyo.

Kwa muda mrefu baraza la halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji limekuwa ikiongozwa na upinzani ambapo kwa sasa baraza hilo litaongozwa na chama cha Mapinduzi CCM mara baada ya kuchukua kata 18 kati ya kata 19 zilizopo katika halmashauri hiyo.

Mwisho.

 

 

Post a Comment

0 Comments