RAIA WA BURUNDI WAKAMATWA WAKIJIHUSISHA NA KILIMO CHA MADAWA YA KULEVYA KIGOMA

 

Kamanda wa Polisi mkoani Kigoma ACP James Manyama

Na Emmanuel Matinde

JESHI la polisi mkoani Kigoma limewakamata watu wanne raia wa nchi jirani ya Burundi kwa tuhuma za kujihusisha na kilimo cha madawa ya kulevya aina ya bangi katika hifadhi ya Wanyama pori ya Moyowosi kando ya Mto Malagarasi wilayani Kibondo kinyume cha sheria.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kigoma ACP James Manyama, alisema, Novemba 8 mwaka huu wakishirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama na idara mbalimbali za serikali, waliwakamata watu hao wakiwa katika mashamba yao ya bangi yenye ukubwa wa ekari 5 ambayo bado haijavunwa na magunia saba ya bangi iliyovunwa yenye uzito wa kilo 134.

Aidha Kamanda Manyama alisema madawa ya kulevya yana athari kubwa kwa jamii ikiwemo kuchochea ongezeko la wagonjwa wa afya ya akili, ongezeko la wategemezi, pia huchangia ongezeko la vitendo vya uhalifu, hivyo polisi wataendelea na operesheni za kuwasaka wote wanaojihusisha na kulima au kuuza madawa ya kulevya.

Hata hivyo Kamanda Manyama alisema polisi wanaendelea na uchunguzi ili kubaini kama kuna watanzania walioshirikiana na watuhumiwa hao na hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi yao.

 

Post a Comment

0 Comments