Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Kassim Majaliwa.
Na Mwandishi Wetu, Dodoma
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameitaka
Wizara ya Maji, Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira jijini Dodoma
(DUWASA) na Sekretarieti ya Mkoa wa Dodoma kuhakikisha mradi wa bwawa la maji
Farkwa uliopo kijiji cha Mombose, wilayani Chemba, mkoani Dodoma unaanza
mapema.
Akizungumza wakati alipotembelea eneo la
mradi huo leo (Jumamosi, Novemba 21, 2020) Waziri Mkuu alisema idadi ya watu
katika mkoa wa Dodoma imekuwa ikiongezeka kwa kasi hivyo ni lazima kuwepo na
chanzo cha maji cha uhakika.
“Mhe. Rais Dkt John Magufuli ameutamka
sana mradi huu wa maji. Hata Ilani ya Uchaguzi imeutaja mradi huu ambao
umetengewa zaidi ya sh. bilioni 900 na utakuwa na uwezo wa kutoa mita za ujazo
128,000 kwa siku. Rais wetu ana nia njema ya kupeleka huduma hii ya maji kote
nchini, tuanze mradi huu mapema,” alisisitiza.
Akizungumzia kuhusu fidia kwa wakazi
watakaoguswa na mradi huo, Waziri Mkuu alisema kuwa waliolipwa fidia ni
asilimia 91 na kwamba kila anayedai atalipwa kwa sababu fedha zipo na hakuna
hata mtu mmoja atakayedhulumiwa.
Aidha, Waziri Mkuu amewahakikishia wakazi
wa eneo hilo kuwa Serikali itasimamia ipasavyo ujenzi wa miundombinu ya huduma
za kijamii ikiwemo shule na huduma za afya katika eneo lililotengwa kabla ya
kuwahamisha na takribani sh. milioni 600 zimetengwa kwa ajili ya shughuli hiyo.
Wakati huohuo, Waziri
Mkuu amemuagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mhandisi Anthony Sanga
ahakikishe wananchi wa eneo hilo wanapewa kipaumbele katika ajira pindi mradi
huo utakapoanza kutekelezwa.
Mapema, Waziri
Mkuu alitembelea chanzo cha maji cha Mzakwe kilichopo nje kidogo ya mji wa
Dodoma na kuagiza mkandarasi ambaye anapaswa kuchimba kisima cha kuzalisha maji
lita 430,000 kwa saa, aanze haraka kazi hiyo ili kuongeza kiwango cha maji
yanayoenda mjini.
0 Comments