TANAPA KUTOA TUZO KWA VYAMA VYA WAANDISHI WA HABARI TANZANIA

Na Mwandishi  Wetu, Dodoma

SHIRIKA la hifadhi za Taifa nchini (TANAPA) limesema litaanza kutoa tuzo kwa klabu za waandishi wa habari nchini ambazo zitaandika habari zenye lengo la kutangaza uhifadhi na Utalii nchini.

Naibu katibu Mkuu wa  Wizara ya Maliasili na Utalii , Dk. Allan Kijazi aliyasema hayo jijini Dodoma wakati akifunga mkutano wa wahariri, viongozi wa taasisi za kihabari na waandishi wa habari waandamizi kutoka vyombo mbalimbali nchini.

Kamishna wa Uhifadhi na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii Dk. Allan Kijazi akifunga mkutano wa wahariri na waandishi waandamizi Tanzania, mkutano uliofanyika jijini Dodoma.

Alisema, awali walikuwa wakitoa tuzo kwa waandishi waliofanya vizuri lakini kulitokea tatizo, tuzo zikasitishwa lakini kuanzia mwakani wataanza kutoa kwa club za waandishi, ambazo waandishi wake watafanya vizuri.

Aidha alisema kuwa,tuzo hizo zitaanza kutolewa ikiwa ni mchango wa kuthamini kazi zitakazokuwa zimefanywa na vyama vya wàndishi wa habari (press clubs) 

Aliongeza kwa kuwataka  viongozi kuwahamasisha waandishi kwenye maeneo yao kuandika habari za uhifadhi na Utalii kwa wingi ili kuelimisha jamii na kutangaza vivutio  vilivyopo nchini.

Kwa upande wake Rais wa Muungano wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) Deogratius Nsokolo alilishukuru Shirika la Hifadhi za Taifa nchini kwa kuendelea kutambua umuhimu wa waandishi wa habari nchini na kuzitumia press club kuhamasisha shughuli za uhifadhi.

Kamishna Msaidizi Mwandamizi Mawasiliano wa TANAPA Paschal Shelutete akimkabidhi cheti Cha ushiriki wa mkutano huo Rais wa Muungano wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania UTPC Deogratius Nsokolo mkutano uliofanyika jijini Dodoma.

Alisema UTPC ipo tayari kushirikiana na TANAPA katika ulinzi wa raslimali za Taifa na uhamasishaji wa shughuli za shirika hilo ikiwa ni pamoja na kuhamasisha Utalii wa ndani na nje pamoja na kukabiliana na ujangili.

Alifafanua kuwa, kuanzishwa kwa tuzo hizo kutawasaidia waandishi kubobea katika uandishi wa habari za uhifadhi na hivyo kuwasaidia wananchi na Taifa kutokana na kuandika habari za kina na zenye tija.

Hata hivyo Nsokolo alitoa wito kwa waandishi nchini kutumia fursa hiyo vizuri ili press klabu ziweze kushindana na kutimiza malengo ya nchi katika uhifadhi.

Shirika la hifadhi za Taifa nchini Tanapa linasimamia hifadhi 22 nchini.

 

 

Post a Comment

0 Comments