WAKULIMA NA WASINDIKAJI WAPATIWA MAFUNZO YA UZALISHAJI NA USINDIKAJI WA MAFUTA YENYE UBORA

Wakulima, wasindikaji, wasambazaji na waraji wa mafuta ya mawese wakiwa kwenye mafunzo ya uzalishaji na usindikaji wa mafuta yenye ubora mkoani Kigoma.


Na Kadislaus Ezekiel Kigoma.

Zaidi ya wakulima, wasindikaji, wasambazaji na waraji wa mafuta ya mawese elfu mbili na mia mbili mkoani Kigoma, wamepatiwa mafunzo ya uzalishaji na usindikaji wa mafuta yenye ubora kwa kuzingatia viwango bora vya vifungashio ili kuongeza thamani ya mafuta ya mawese.

Mkurugenzi wa udhibiti ubora kutoka shirika la viwango Tanzania TBS Lazaro Msasalaga alisema mafuta ya mawese yanayozalishwa hayakidhi viwango vya ubora kutokana na uzalishaji usiozingatia technologia ya kisasa katika kuchakata mafuta.

Alisema wazalishaji wengi wa mawese wamekuwa wakitumia njia za asili ambazo si bora na kwamba mafuta mengi yanakuwa na maji na hivyo kuchangia athali kwa walaji wanaotumia mafuta ya mawese.

Aidha Festo Kapela ambaye ni mkufunzi kutoka Wizara ya Viwanda na Biashara alieleza mbele ya wachakataji na wakulima wa mazao ya mafuta kuwa, asilimia 80 ya mafuta yanayotumika nchini hutoka nje ya nchi na kwamba ikiwa mafuta ya mawese yatapewa ubora tangu kuandaliwa yataongeza thamani katika soko la ushindani.

"Nchi za Afrika Mashariki na kati zinategemea sana mafuta ya nje ambapo kama viwanda vitaboreshwa vya kuchakata mafuta ya mawese na kuongezwa ubora itakuwa fursa kwa wakulima kuongeza pato la Taifa kupitia soko la mafuta" alisema Kapela.

Kwa upande wake Kaimu Mkuu wa TBS Kanda ya Magharibi Rodney Alananga alisema  katika tathimini ambayo imefanyika wamebaini mafuta ya mawese yanayotumika kutokuwa na ubora unaotakiwa ikitokana na uzalishaji duni unaofanywa na wakulima.

Hatahivyo baadhi ya wakulima akiwemo Isaya Rashidi, na Neema Juma ambaye ni mchakataji mafuta ya mawese wameomba serikali kuwezesha upatikanaji wa vifungashio na kupunguza bei ili kuendana na hali ya uchumi kwa wakulima.


 


Post a Comment

0 Comments