CPCT KIGOMA YAIOMBA SERIKALI KUFANYA UKAGUZI MADHUBUTI ILI KUDHIBITI UGONJWA WA CORONA

 


Na Emmanuel Michael Senny

Umoja wa makanisa ya Kipentekoste mkoani Kigoma CPCT umeitaka serikali kufanya ukaguzi makini unaoshirikisha wananchi ili kudhibiti njia zote zinazoweza kupelekea ugonjwa wa Corona kuenea kwa kasi huku wakiitaka serikali kutoa elimu zaidi ya Virusi vya Corona ili wananchi waelewe na kufahamu njia sahihi za kujikinga na ugonjwa huo

Hayo yalijiri wakati wa maombi ya kuliombea Taifa la Tanzania ili Mungu aliepushe na ugonjwa hatari wa Corona ambao umeenea duniani kote.

Akisoma risala kwaniaba ya CPCT, Katibu wa CPCT ambaye pia ni Askofu Mtaafu na Mchungaji wa Kanisa la PAG Katubuka Michael Kulwa alisema pili wamefanya mkutano wa maombi maalumu kwaajili ya kuombea mkoa na nchi ya Tanzania ili Mungu aepushe na virusi vya corona.

Aidha alisema kuwa serikali na vyombo vinavyohusika wawe na ukaguzi makini kwa wageni na wenyeji wanaoingia na kutoka nchini pia serikali itoe vifaa vitakavyobaini washukiwa wa ugonjwa  huo hatari.

Aliongeza kuwa serikali ni vema ikatoa elimu dalili na namna ya kujikinga na ugonjwa wa Corona ili iwe rahisi hata endapo mtu ataambukizwa itakuwa rahisi kutambua na namna ya kutoa taarifa sehemu husika haraka zaidi.

Naye Katibu Tawala  Msaidizi  wa Mkoa  wa Kigoma  akimuwakilisha Katibu Tawala wa mkoa huo Ndg Vedasto Makota alisema serikali ya mkoa inaendendelea kujidhatiti katika kukabiliana na ugonjwa huo hasa kuweka vifaa katika maneo yote ya mipakani ikiwemo viwanja vya ndege.

Aliongeza kwa kuwataka viongozi wa dini kuchukua hatua za msingi za kuwaelimisha waumini wao kufuata kanuni za afya huku akisema serikali nayo itaendelea kutoa elimu kwa wananchi wake.

Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Dr. Saimon alisema sekta ya afya ya mkoa inaendelea kuchukua tahadhali ikiwemo kutoa elimu kwa wananchi ili wazifahamu dalili za ugonjwa huo ikiwemo njia sahihi za kujikinga ikiwemo kuvaa barakoa na kunawa mikono kwa maji tiririka kila wakati.

 

Post a Comment

0 Comments