WANANCHI KIGOMA WATAKA ELIMU ZAIDI KUHUSU UGONJWA WA CORONA

 


Na Mwandishi Wetu, Kigoma

CORONA ni ugonjwa wa Homa kali ya mapafua ambao kwa kitaalamu unaitwa COVID19 na uligundulika kwa mara ya kwanza nchini China mwishoni mwaka 2019, Ugonjwa huo ulianza kuenea kwa kasi kutoka nchini china na kuingia katika nchini nyingine duniani.

Wakati Ugonjwa huo ukisumbua nchini nyingi duniani kwa upande wa Tanzania ulichelewa kuingia ikiwa ni baada ya jitihada madhubuti za kudhibiti ugonjwa huo zilizowekwa na serikali kupitia wizara ya afya maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto iliyokuwa chini ya Waziri Ummy Mwalimu.

Aidha hata ulipoingia kwa kisa cha kwanza kutangazwa bado serikali ilimudu kuudhibiti ugonjwa huo, ambapo aliyekuwa Rais wa Tanzania Hayati John Pombe Magufuri aliwahimiza watanzania kufunga na kuomba kila mmoja kwa imani yake ili ugonjwa huu utokomee.

Wakati serikali ikiendelea kupambana na ugonjwa huu ikiwemo kuwahimiza wananchi kufuata kanuni za afya na maelekezo kutoka Wizara ya Afya baadhi ya wakazi mkoani Kigoma wameonekana kutofahamu dalili za ugonjwa huo huku wakiitaka serikali kutoa elimu zaidi kwa wananchi sambamba na kurahisisha upatikanaji wa vitakasa mikono pamoja na barakoa.

Wananchi hao akiwemo Siwema Hamis, John Amran na Sudi Majidi walisema kuwa kutokujua dalili za ugonjwa huo inawapa wakati mgumu kutoa taarifa za ugonjwa jambo linaloweza kupelekea ugonjwa kuenea pindi atakapopatikana mtu mwenye maambukizi wakati jamii haifahamu dalili zake.

“Tunashindwa kutoa taarifa mana kila ukimuangalia mwenzako unahisi yuko salama ila kama tukifahamu dalili zake itakuwa nafuu kwetu kutoa taarifa za ugonjwa ikiwemo kukaa mbali na mtu mwenye maambukizo” walisema.

Wakizungumzia njia za kujikinga wananchi hao walisema kuwa hawafahamu njia za kujikinga japo baadhi yao wanaonekana kufahamu njia za kujikinga na ugonjwa huo.

“Sisi tunaiangalia serikali, ni vyema ikatuma wataalamu wakapita mitaani au hata kwenye mikusanyiko ya watu na kutoa elimu ya namna sahihi ya kujikinga na corona tofauti na hapo tutajikuta tunaambukizana tu bila kujua na kuanza kufa mmoja mmoja” waliongeza.

Dkt Ambakise Muhiche ni Afisa Afya wa mkoa wa Kigoma kwa upande wake alisema suala la elimu kwa wananchi linafanyika ikiwemo kusambaza vipeperushi mitaani na maeneo yote yenye mikusanyiko ya watu  vyenye elimu ya kujikinga na ugonjwa huo ikiwemo dalili zake hivyo wananchi wasome vipeperushi hivyo.

“Elimu inatolewea sana kama nilivyozungumza ila niwashauri tu wananchi kusikiliza vyombo vya habari ambapo huwa tunakuwa na vipindi vya kuelimisha jamii kuhusu ugonjwa huu, lakini pia wananchi waache tabia ya kusikiliza elimu ambazo zinapotosha kutoka kwa watu ambao sio wataalamu wa afya.

“Kuhusu dalili za Ugonjwa huu kwa kifupi ni pamoja na kukohoa, kichwa kuuma pia kuwa na joto kali lakini mafua yasiyo ya kawaida, ukiona hivyo fika haraka katika vituo vya kutolea huduma za afya” alisema Dkt Ambakise.

Aidha Dkt Ambakise alisema kuwa njia za kujikinga ni pamoja na kutenga ndoo ya maji tiririka kwaajili ya kunawa mikono mara kwa mara, kutumia vitakasa mikono, kufunika pua na kiwiko cha mkono wakati wa kupiga chafya sambamba na kuepuka kukaa sehemu za mikusanyiko na kama kuna ulazima basi tuvae bakoa

“Kwa kufuata njia hizo kwa pamoja tunaweza kupambana na maambukizi ya ugonjwa wa Corona” alisisitiza Ambakise.

Post a Comment

0 Comments