WANANCHI WATAKIWA KUZINGATIA USAFI WA MAZINGIRA ILI KUEPUSHA MAGONJWA YA MLIPUKO



Na Mwandishi Wetu, Kigoma

Idara  ya  Afya  Halmashauri  ya  Wilaya  Kigoma  imewataka wananchi  waishio mwambao wa Ziwa Tanganyika kuzingatia usafi wa mazingira yanayowazunguka kwa kipindi hiki ambacho mvua zimeanza kunyesha ili kudhibiti mlipuko wa magonjwa  kama vile kipindupindu.

Hayo yanajiri wakati Tanzania ikiendelea na mapambano dhidi ya magonjwa ya mlipuko ambayo yamekuwa yakikwamisha shughuri za maendeleo kwa wananchi ambao huchukua muda mwingi kutafuta tiba badala ya kufanya kazi.

Afisa afya wa Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma Saulo Mshale, alisema vijiji vilivyopo pembezoni mwa ziwa Tanganyika vimekuwa vikiandamwa na magonjwa ya kuhara kutokana na mazingira machafu na kutozingatia kanuni za afya.

Wananchi wengi wa pembezoni mwa ziwa hawafuati kanuni za afya ikiwemo kuwa na vyoo bora, kutumia maji machafu na kushindwa kuweka mazingira katika hali ya usafi jambo linalosababisha magonjwa ya mlupuko ikiwemo kuhara na kipindupindu hasa kipindi hiki cha mvua” alisema.

Ameongeza kuwa wananchi wamekuwa wakitumia maji ya ziwa bila ya kuyachemsha, lakini pia wengi wao hawana vyoo jambo linalowafanya kujisaidia vichakani lakini pia kukaa kwenye mazingira machafu kwao ni kawaida.

Aidha Mshale alisema kuwa sekta ya afya imetuma  wahudumu wa afya ngazi ya jamii kutembelea kila kaya kwa lengo la kutoa elimu kwa wancnhi na kuhakikisha wananchi wanafuata kanuni za afya.

“Imebidi tufanye hivyo ili kuhakikisha tunatokomeza magonjwa ya mlipuko katika vijiji vilivyopo pembezoni mwa ziwa kwa kutuma wataalamu” Aliongeza

Kwa upande wao wananchi waishio mwambao wa ziwa Tanganyika wameiomba serikali kuweka mikakati ya kutoa elimu ya namna ya kufuata taratibu za kiafya.

“Huduma za afya zipo lakini sio kwa kiwango kikubwa lakini tumekuwa tukienda katika vituo vya afya tukiwa tayari tuna wagonjwa, sasa ni vyema serikali ikaja kutoaelimu ili tujue tunajikinga vipi na ugonjwa wa kuhara” walisema.

Kwasasa maeneo mengi ya mkoa wa Kigoma mvua imekuwa ikinyesha kila wakati hivyo kwa maeneo ambayo mazingira ni machafu kumekuwa na hatari ya kupata magonjwa ya mlipuko jambo ambalo serikali imeanza kulifanyia kazi

 


Post a Comment

0 Comments