ASILIMIA 58 YA WAZAZI MANISPAA YA KIGOMA UJIJI WANANYONYESHA KWA MIEZI 6 MFULULIZO

 


Na Mwajabu Hoza , Kigoma.

IMEELEZWA kuwa asilimia 58 ya wazazi katika Manispaa ya Kigoma Ujiji mkoani Kigoma wananyonyesha watoto wao kwa kipindi cha miezi sita mfululizo bila kuchanganya na chakula chochote na idadi kubwa ni wazazi walio katika sekta rasmi za ajira.

Kaimu mratibu wa lishe Manispaa ya Kigoma Ujiji Pendo Samizi ameeleza kuwa kwa mujibu wa sera na sheria mzazi anatakiwa kupata likizo ya uzazi ya siku 84 mara baada ya kujifungua ili aweze kupata fursa ya kunyonyesha lakini pia kulea vyema mtoto wake.

“Likizo inapokamilika mzazi anakuwa na ruhusa ya kwenda nyumbani kunyonyesha kwa kipindi hicho cha miezi sita na lengo ni kuhakikisha mtoto hapatiwi chakula ama maziwa tofauti na maziwa ya mama yake” .

Mara kadhaa sheria imekuwa ikiwalenga wale waliopo kwenye ajira rasmi hususan waliopo serikalini lakini wale waliopo katika sekta binafsi zenye mlengo wa kibiashara  imekuwa vigumu kuzingatia taratibu za unyonyeshaji wa mtoto na wengi wao wanaanza kuwapatia watoto chakula ama maziwa ya kopo na ya ng’ombe hali ambayo ni hatari kwa afya ya mtoto.

 “Na hii linachangia wanawake  kukosa fursa za ajira katika taasisi na sekta binafsi wakihofia kupoteza uzalishaji mali kipindi ambacho mama atakuwa amejifungua na hivyo ajira nyingi zikifanywa na wanaume”amesema

Alisema serikali inatakiwa kutilia mkazo na kusimamia sheria iliyopo ili watoto wapate haki zao za kupata lishe iliyobora kutoka mzazi ambapo hili litasaidia kuondoa changamoto ambazo watoto wanaweza kuzipata endapo hawatanyonya vizuri maziwa ya wazazi wao.

Pendo alisema endapo mtoto atakosa maziwa ya mama kwa kipindi cha miezi sita mfululizo atakuwa amekosa baadhi ya virutubisho na kusababisha kupata matatizo ya kiafya ikiwemo njia ya hewa, upungufu wa damu mwilini, kutokuwa na uwezo wa kiakili darasani lakini pia kupungua kwa mahusiano ya karibu kati ya mama na mtoto.

Katika hatua za awali wameendelea kuelimisha jamii, wadau na kuishauri serikali kuangalia namna ya kusimamia sera na sheria ili kila mtoto anayezaliwa aweze kupata haki ya kunyonya vizuri ili kuondokana na magonjwa yanayoweza kujitokeza kwa mtoto.

Hata hivyo wanaume nao wametakiwa kuwa mstari wa mbele kuhakikisha wanawasaidia wazazi kuweza kunyonyesha watoto wao kwa kipindi chote cha miezi sita ikiwa ni pamoja na kuwapatia lishe bora kabla ya kujifungua na baada ya kujifungua ili waweze kuwa ma maziwa mengi ya kunyonyesha watoto wao.

 

Post a Comment

0 Comments