MIUNDOMBINU YA BARABARA NGURUKA BADO CHANGAMOTO, SERIKALI YATOA NENO



Na Mwajabu Hoza, Kigoma

Changamoto ya miundombinu ya barabara katika kata ya Nguruka wilaya ya Uvinza mkoani Kigoma imeelezwa kuwa kikwazo cha wakazi wa kata hiyo kushindwa kufanya shughuli za uzalishaji mali ikiwemo kilimo na biashara hususan wakati wa masika kutokana na kukatika kwa miundombinu ya barabara na kusababisha madimbwi ambayo ni hatari kwa usalama wao.

Wakitoa kero zao mbele ya mkuu wa Mkoa Kigoma Thobias Andengenye wananchi hao wamesema barabara zilizopo kwenye kata ya Nguruka ambazo zinaunganisha maeneo mengine zimekuwa hazipitiki hasa katika kipindi cha masika na hivyo kuiomba serikali kuwatatulia changamoto hiyo.

Feruzi Shabani ambaye ni mwenyekiti wa Kitongoji na Wakawaka Kafulila walisema wakati wa masika barabara hazipitiki na hivyo kusababisha hata shughuli za uzalishaji mali kukwama, vitongoji kutengenishwa na hivyo kukosa mawasiliano baina ya kitongoji na kitongoji .

Akizungumzia ujenzi wa barabara Mhandisi Richard Maganga Kutoka TARURA wilaya ya Uvinza alisema barabara zinazounganisha kata ya Igalula, Itebula na Mganza zipo katika mkakati wa ujenzi kwa kipindi cha mwaka 2021/2022.

Alisema barabara hizo awali zilikuwa zimetengewe kiasi cha shilingi milioni 30 hadi 50 lakini kwa sasa serikali imetenga milioni 140 kwa ajili ya kuhakikisha barabara ambazo zinachangamoto zinafanyiwa matengenezo na kuendelea barabara ambazo ni mpya zilizoibuliwa.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Uvinza Jackson Mateso alisema hakuna kata ambayo itabaguliwa katika uboreshaji wa miundombinu ya barabara ikiwemo ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami kata zote zinahaki sawa ya kupata maendeleo.

Post a Comment

0 Comments