WAZAZI NA WALEZI WATAJWA KUWA CHANZO CHA UTORO KWA WANANFUNZI KIGOMA

 


Na Emmanuel Michael, Kigoma

Utoro kwa wanafunzi wa shule za msingi kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma mkoani Kigoma umeelezwa kuchangiwa na baadhi ya  wazazi na walezi kuwatumikisha watoto wao kwenye shughuli za kilimo wakati wa msimu wa masika.

Kituo hiki kimezunguka katika baadhi ya shule za msingi kwenye Halmashauri ya wilaya ya Kigoma ikiwemo shule ya Msingi Kiganza na kuzungumza na Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo Said Nshoye ambaye ameeleza kuwa kipindi cha msimu wa masika wazazi na walezi wamekuwa wakiwapeleka watoto wao shamba kwa lengo la kuwasaidia shughuli za kilimo.

Amesema tabia hiyo imekuwa ikichangia utoro wa wanafunzi kila ifikapo msimu wa masika na kuadhiri maendeleo ya kielemu na hata kiwango cha ufaulu  kwa wanafunzi hao kushuka kutokana na kutohudhuria vipindi vya masomo darasani.

Nshoye amesema changamoto ya utoro inaadhari kubwa kwa wale wa elimu ya awali ambao wanatakiwa kujua (KKK ) kusoma, kuandika na kuhesabu ikiwa ni msingi wa elimu kwa wanafunzi jambo linalochangia wanafunzi wengi kiwango chao cha elimu kuwa chuni.

“Tatizo kubwa ni pale ambapo wale watoto wenye umri mdogo wanaosoma  chekechea hadi darasa la tatu mara nyingi hubaki nyumbani pale wanapoona dada ama kaka zao hawaji shule na wao hawaji na hilo linawajengea tabia ya utoro tangu wakiwa wadogo” amesema  

Wakizungumza na Blog hii na baadhi ya wanafunzi akiwemo Ismail Hamza, Ashura Issa wamekiri kuwepo kwa tabia ya wazazi kuwatumikisha kwenye shughuli za kilimo pamoja na kazi za nyumbani huku wakiwazuia kwenda shule.

“Wakati wa masika wazazi wamekuwa wakituzuia kwenda shule ili tukawasaidie shughuli za kilimo shambani na  wakati mwingine tunapewa kazi za nyumbani muda ambao tunatakiwa kwenda shule kusoma na hilo linasababisha sisi kuwa watoro shuleni” walisema wanafunzi hao

Wakitoa maoni yao wananfunzi hao wamesema elimu ni msingi wa maisha hivyo wamewaomba wazazi na walezi kuwapatia nafasi ya wao kupata fursa ya masomo bila kujali msimu wa kilimo jambo litakalochangia wao kufikia malengo yao sambamba na wadogo zao ambao wanasoma elimu ya awali.

Wakizungumzia hilo wazazi akiwemo Delifina Simon na Astelia Patrick wamesema hakuna ukweli wowote wa wazazi kuwa chanzo cha watoto kutokwenda shule bali kumekuwa na tabia ya watoto wenyewe kujificha porini ama kwenda mtoni kuoga jambo linaloathiri hata wadogo zao wanaosoma elimu ya awali mana wanaona kile wanachofanya wakubwa zao.

“ Watoto wengi ni waongo wanaaga asubuhi wanaenda shule hawafiki wanaishia maporini kudandia miti ya matunda na wengine wanakwenda mtoni kuoga hata muda huu ukiingia porini utawakuta muda ukifika wa kurudi nyumbani nao wanarudi” walisema

Mwenyekiti wa Kijiji hicho Abel Godfrey amesema suala la kutumikishwa watoto katika kijiji hicho lilikuwepo ambapo serikali ya kijiji imejipanga kuwachukulia hatua za kisheria wazazi ambao watabainika kuwatumikisha watoto wao katika shughuli zao za utafutaji mali katika familia na kutoa wito kwa wazazi, walezi na walimu kujenga tabia ya mawasiliano ya vikao vya mara kwa mara ili kujua maendeleo ya elimu kwa watoto wao.

“Ufuatiliaji unatakiwa kuanzia kwa wale watoto wa elimu ya awali mana ndiko kwenye msingi wa maendeleo ya mtoto kuipenda shule na kuwa na maendeleo mazuri kielimu” alisema.

Post a Comment

0 Comments