WANAUME WATAKIWA KUJITOKEZA KUPIMA AFYA

 


Na Mwajabu Hoza, Kigoma

HALI ya maambukizi ya virusi vya Ukimwi mkoani Kigoma imeelezwa kupungua na kufikia asilimi 2.9 jambo ambalo limeelezwa kuchangiwa na wananchi kujitokeza kupima afya zao na  changamoto ikibaki kwa wanaume kutojitokeza kupima afya.

Taarifa za awali zinaonyesha hali ya maambukizi ya virusi vya ukimwi ni asilimia 3.4 hali iliyokuwa ikichangiwa na jamii kutokuwa na uelewa wa kujitokeza kupima ili kuweza kupata huduma mapema na kupunguza hali ya maambukizi mapya.

Matumizi ya dawa za kupinguza makali ya virusi vya ukimwi imeelezwa kuendelea kupunguza hali ya maambukizi kwa mkoa wa Kigoma ambapo wanaojitokeza kwa wingi kupima wamekuwa ni wanawake.

Hali hii imekuwa ikichangia baadhi ya wanaume kuamini kuwa wenza wao wakipima inakuwa imetosheleza na kutoona sababu ya wao kupima jambo ambalo limeelezwa kuwa ni hatari hususani wakati wenza wao wakiwa na  mjamzito.

Taarifa zinaeleza endapo mama atakuwa na maambukizi ya virusi vya ukimwi kuna uwezekano wa kumuambukiza mtoto kabla na wakati wa kujifungua lakini pia wakati wa kunyonyesha hivyo ipo sababu ya wazazi kupima afya zao ili kuhakikisha wanachukua tahadhari za kiafya kwa mtoto anayetarajia kuzaliwa.

Wataalamu wa afya wanaeleza kuna uwezekano wa mtoto kupata maambukizi kutoka kwa mama akiwa tumboni na hilo linaweza kujitokeza endapo atuagusishwa na damu ama majimaji kutoka kwa mama lakini pia wakati wa kunyonya endapo mama atakuwa na vidonda.

Akizungumzia ushiriki wa wanaume wakati wa siku ya Ukimwi duniani mratibu wa Ukimwi  Dkt,Hosea William amesema licha ya kupungua kwa kiwango cha maambukizi ya virusi vya Ukimwi ukilinganisha na mikoa mingine pamoja na ile ya kitaifa ya asilimia 4.7 bado tabia ya wanaume kutopima afya zao imekuwa ikichangia hatari ya afya kwa wenza wao.

Dkt. Hosea amesema hatua ya kupungua kwa maambukizi ya virusi vya ukimwi inatajwa kuwa ni juhudi za serikali Pamoja na wadau kuhakikisha elimu na umuhimu wa kupima afya kuwa ni kipaumbele katika mapambano dhidi ya virusi hivyo lakini pia wanaobainika kuanza kupata dawa mapema.

Staphord Chamgeni na Dkt,Beatres Mtesigwa wameeleza kuwa bado jitihada zinaendelea za kutoa elimu kwa jamii hususani wanaume ili kuona umuhimu wa kupima afya zao na kuacha tabia ya kujinyanyapaa wenyewe.

Asilimia 74.7 ya wanaume mkoani Kigoma ndio hujitokeza kupima huku wanawake ikiwa ni asilimia 88.7  ambapo wanawake wengi hujitokeza kupima kwa maslahi ya kulinda familia zao ikiwemo watoto huku wanaume wakibaini kuwa mwanamke anatatizo la VVU huwa wanawatelekeza wenza wao pamoja na watoto.

 

Post a Comment

0 Comments