WIZARA YA MIFUGO NA UVUVI KUKABILIANA NA UPOTEVU WA MAZAO YA UVUVI ZIWA TANGANYIKA



Na Mwajabu Hozza, Kigoma

WIZARA ya mifugo na uvuvi imekuwa ikichangia pato la Taifa kwa asilimia 1.7 kiwango ambacho kimeelezwa kuwa kidogo ukilinganisha na rasilimali zilizopo na hivyo wizara kuja na mpango mkakati wa kukabiliana na upotevu wa mazao ya uvuvi pamoja na kuongeza uwekezaji kwenye sekta hiyo.

Kauli hiyo imetolewa na katibu mkuu wizara ya mifugo na Uvuvi Rashid Tamatamah wakati wa warsha ya wadau wa mradi wa FISH4ACP ambao utaanza  2022 /2024 na umelenga kuboresha mnyororo wa thamani Kwa mazao ya samaki na dagaa.

Amesema katika mpango wa tatu wa maendeleo ya Taifa kwa mwaka 2021 mpaka 2026  sekta ya uvuvi imejipanga kuongeza pato la Taifa na kufikia asilimia tatu kwa kufanya maboresho mbalimbali ikiwemo kuwezesha miundombinu yote inayohusiana na sekta ya Uvuvi , ununuzi wa meli nne pamoja na kuwaunganisha wavuvi na wachakataji wa mazao ya Uvuvi kwenye taasisi za kifedha ili waweze kupata mikopo.

Mkurugenzi wa Uvuvi wizara ya mifugo na uvuvi Ummanuel Bulayi amesema ili mradi wa FISH4ACP uwe na tija lazima wadau wote wa sekta ya uvuvi kushirikiana kwa pamoja kutokomeza uvuvi haramu kwenye maziwa makuu jambo litakalochangia kuwa na uvuvi endelevu katika Ziwa Tanganyika mkoani Kigoma .

Aidha Katibu Tawala mkoa wa Kigoma Rashid Mchatta amesema  mradi huo ambao unalenga kanda za Afrika utakuwa na fursa nzuri ya kuufungua mkoa wa Kigoma kiuchumi  kupitia rasilimali zilizopo.


Baadhi ya washiriki  wameeleza changamoto zinazowakabili katika shughuli zao za uvuvi na uchakataji wa mazao ya samaki na dagaa kuwa ni pamoja na kutokuwepo kwa bei elekezi za samaki na dagaa pamoja na ukosefu wa masoko na hivyo kuchangia hali  ya kipato kuwa chini huku wakipongeza serikali kwa mradi uliowafikia ambao utasaidia upatikanaji wa mikopo.

 


Post a Comment

0 Comments