KIGOMA YAHAMASHISHWA KUHUSU ZOEZI LA UTOAJI WA CHANJO YA POLIO


Na Mwajabu Hoza, Kigoma.

WATAALAM wa Afya mkoani Kigoma wameeleza kufanya uhamasishaji katika jamii kuhusu zoezi la Utoaji wa Chanjo ya Polio kwa Watoto walio na umri chini ya miaka 5 ili kuhakikisha huduma inatolewa kikamilifu kwa lengo la kupambana na maambukizi ya Ugonjwa huo.

 
Zoezi hilo la chanjo ya Polio linatarajiwa kuanza tarehe 28 ya April hadi Mei mosi ya mwaka huu ambapo takribani watoto 547,000 watafikiwa na huduma ya chanjo na watoto wengine Elfu 42 kutoka Kambi za wakimbizi Za Nduta na Nyarugusu Mkoani Kigoma.
 
Akizungumza hatua hiyo ya utoaji wa chanjo kwa watoto walio na umri chini ya miaka mitano Mganga mkuu wa Mkoa wa Kigoma Dkt Jesca Lebba amesema zoezi hilo linaendana sambamba na utoaji wa elimu juu ya umuhimu wa chanjo kwa watoto hao ambapo elimu hiyo itahusisha zaidi wazazi na viongozi ili kuhakikisha zoezi linafanikiwa.

Amesema zoezi la chanjo limekuja katika jamii mara baada ya kutokea kwa mlipuko wa ugonjwa huo katika eneo la Lilogwe nchini Malawi na kuna uwezekano mkubwa wa kusambaa na kuadhiri maeneo mengine na hivyo serikali ikaona ipo sababu ya kuanza kutoa chanjo hiyo kwa watoto.

“Ugonjwa huu ni virusi ambavyo huambukizwa kupitia kinyesi na hauna tiba isipokuwa chanjo na unashambulia mishipa ya  fahamu na unaweza kusababisha mtoto kupooza na tiba yake pekee ni chanjo pekee ambayo haina madhara yoyote kwa mtoto na tunaitoa chanjo hii kwa sasa kutokana na mlipuko uliojitokeza" Amesema Jesca Lebba   

Amesema maeneo ambayo yatatiliwa mkazo zaidi ni maeneo ya mipaka ambayo yapo katika hatari kubwa ya maambukizi kutokana na jamii ya maeneo hayo kuwa na muingiliano mkubwa wa watu ambao wanaingia na kutoka nchini.

Jesca amesema chanjo hiyo ni muhimu na  itatolewa kwa njia tofauti tofauti ikiwemo nyumba kwa nyumba , kwenye vituo vya kutolea huduma , pamoja na maeneo ya shuleni ambapo wahudumu wa afya watafika kwenye maeneo yote muhimu ambayo watoto wanapatikana.
 
Kwa upande wa wadau wa afya wakiwemo shirika la Afya Duniani WHO Dkt Gerald Marwa ameeleza ili kuhakikisha zoezi hilo linafanikiwa na kufikia lengo lililokusudia na serikali ni lazima elimu itolewe ili kuondoa imani potofu iliyopo ndani ya jamii kuhusu chanjo hiyo na sababu zinazosababisha kutolewa kwa sasa.
 
Hata hivyo katika utekelezaji wa mpango Jumuishi wa Taifa wa malezi, Makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto PJT-MMMAM wa Mwaka  2021/2022 hadi 2025/2026 serikali imeendelea kutoa huduma bora za afya kwa maendeleo na ukuaji timilifu wa watoto kwenye masuala ya chanjo na dawa za minyoo kwa  lengo la kuwakinga watoto na maambukizi ya magonjwa mbalimbali.

Imeelezwa kuwa chanjo za watoto nchini Tanzania zimetolewa kwa zaidi ya asilimia 95 na hilo linatokana na muamko wa jamii kutambua umuhimu wa watoto kupata chanjo kupitia elimu inayotolewa na wataalamu wa afya.
 
 
Mkuu wa mkoa wa Kigoma Thobias Andengeye akatoa msisitizo kwa watumishi wa serikali kutokuwa kikwazo katika utekelezaji wa zoezi hilo na kuwataka watumishi wote kwa nafasi zao walizonazo kulisimamia vyema zoezi hilo kwa maslahi ya watoto na taifa kwa ujumla.
 
 “Watoto wetu hawawezi kuadhirika kwa hili , tunatakiwa kuwa mstari wa mbele katika kampeni hii kuhakikisha tunawatetea na kuwakinga watoto hawa ambao ni malaika wasio na uwezo wa kujitetea wao wenyewe hivyo ni jukumu letu kuwatetea kwa kuhakikisha kila mtoto anapata chanjo hii ili tuweze kuwa na Taifa lenye nguvu hapo badae”

Baadhi ya wananchi wametoa maoni yao juu ya chanjo hiyo ambapo wamesema kuna umuhimu mkubwa kwa watoto kupatiwa chanjo ya Polio kwa kuwa wapo katika hatari kubwa ya kupata maambukizi 

" Watoto wetu wadogo mara nyingi wanacheza hovyo maeneo mbalimbali na ugonjwa huu unasambaa kupitia njia mbalimbali hivyo katika michezo yao anaweza kupata maambukizi lakini kama atakuwa ameshapata chanjo itakuwa vigumu kwa mtoto kupata adhari kupitia ugonjwa huu" 

Aidha walitoa ushauri kwa serikali kuhakikisha watoto wote wanapata chanjo ikiwa ni pamoja na kuwafikia wale waliopo majumbani kutokana na baadhi ya wazazi kuacha kuwapeleka watoto wao cliniki kupata huduma mbalimbali ikiwemo chanjo. 

 


Post a Comment

0 Comments