Na Anthony Kayanda, Kigoma.
Ushiriki duni wa wanaume katika elimu ya uzazi wa mpango ni
mojawapo ya chanzo cha umasikini katika kaya nyingi, hususani kwa watu
wanaoishi vijijini.
Hayo yameelezwa na mratibu wa asasi ya Tanzania Participatory
& Rural Development Organization (TAPRUDO), Eunice Katabwa alipokuwa
akizungumza na waandishi wa habari mjini kigoma.
Amesema wanaume wengi wamekuwa na mtazamo hasi wa kushiriki
masuala ya uzazi wa mpango ambapo wanadhani jukumu hilo ni la wanawake pekee.
"Tumekutana na baadhi ya wanaume wakati wa kuelimisha jamii
juu ya mambo mbalimbali na mtambuka lakini wengi wamekuwa wakisema mambo ya
uzazi wa mpango ni ya wanawake, dhana hii ni mbaya na lazima wanaume
waelimishwe kujua athari yake," alisema Eunice.
Amesema kutokana na wanaume hao kutojua faida ya kuzaa kwa mpango
matokeo yake ni kuwasababishia madhara ya kiafya kinamama kwani wengi
wamejikuta wakizaa maravkwa mara.
"Utamkuta mama mwaka huu anabeba mimba na mwakani mtoto,
akinyonyesha mwaka mmoja mimba nyingine, sasa katika mazingira ya aina hii
unategemea huyu mama atapata muda wa kuzalisha mali na ukizingatia wengi ni
wakulima huko vijijini? amehoji Eunice.
Ili kuleta maendeleo katika jamii lazima familia nzima
washirikiane katika kazi ya uzalishaji mali, hivyo lazima mama awe na nguvu ili
azalishe kikamilifu.
Ametoa mwito kwa taasisi na mashirika mbalimbali kutoa elimu ya
uzazi wa mpango kwa wanaume kwani wakifahamu vizuri itasaidia kupanga uzazi na
hivyo afya ya wanawake itaimarika.
Baadhi ya watu waliotoa maoni kuhusu wanaume kupata mafunzo ya
uzazi wa mpango wamesema jambo hilo ni muhimu kwa vile litapunguza migogoro
katika familia na litaongeza ushirikiano katika uzalishaji mali.
Mkazi wa kijiji cha Msimba, Awamu Hussein amesema wanaume wengi
hawana utaratibu wa kuwasindikiza wake zao kliniki, hivyo elimu ya uzazi
inayotolewa na wauguzi inaishia kwa wanawake tu.
"Ikiwa na sisi wanaume tutakwenda kliniki na wake zetu
itasaidia kujua changamoto zinazowakabili wanawake kuanzia wakati wa mimba,
kujifungua hadi kunyonyesha," amesema Hussein.
Amesema kuzaa mfululizo na mara kwa mara kunamfanya mwanamke
achoke na kupoteza uwezo wa kufanya kazi hususani kilimo ambayo ndio uti wa
mgongo kwa wakazi wengi wa vijijini.
Kuruthumu Maulidi wa Katubuka mjini Kigoma amesema wanaume wengi
wanaona haya kufuatana na wenza wao kliniki kwa madai kwamba mambo ya kliniki
hayawahusu.
Amesema wengi wanalazimika kwenda na wenza wao siku ya kwanza mama
anapoanza kliniki kwa sababu ni lazima apimwe vipimo vingi vya afya ambayo ni
lazima pia mwanaume ahusishwe.
"Baada ya hapo humuoni tena mwanaume kwenda kliniki lakini
(wanawake) tumezoea na tunaona ni suala la kawaida tu," alisema.
John Daudi wa Majengo mjini Kigoma amesema itakuwa jambo gumu kwa
wanaume kushiriki mambo ya uzazi kwa sababu elimu hiyo inatolewa zaidi kliniki.
Ametaka serikali iweke utaratibu wa kutoa elimu ya uzazi wa mpango
hadi mahali pa kazi ili iwe rahisi wanaume wengi kufikiwa badala ya kutegemea
waende kliniki na wake zao.
Mkoa wa kigoma ni mojawapo ya mikoa inayoendelea kutoa elimu ya
afya ya uzazi na uzazi salama kwa jamii kupitia serikali na mashirika binafsi
na asasi za kiraia.
0 Comments