MKOA WA KIGOMA KUVUKA LENGO LA UTOAJI WA CHANJO YA POLIO

 


Na Mwajabu Hoza, Kigoma.

 

MKOA wa Kigoma umetoa chanjo ya Polio 642,714 kwa watoto chini ya umri wa miaka mitano ikiwa ni sawa na asilimia 107 na lengo likiwa ni kupambana na virusi vya ugonjwa huo kwa watoto.

 

Akizungumzia hilo Mganga mkuu wa mkoa wa Kigoma Jesca Lebba amesema makisio ya mkoa ilikuwa ni kutoa chanjo kwa watoto 593, 277 ambapo hadi kukamilika kwa zoezi la utoaji wa chanjo ya Polio kulikuwa na ongezeko la watoto 49,437 waliopata chanjo hiyo.

 

Amesema mkoa ulitenga vituo maalumu vya kutolea chanjo pamoja na maeneo ya kutolea huduma za afya ambapo jumla ya vituo 256 vilitumika kutoa chanjo hiyo kwa watoto, maeneo ambayo jamii iliweza kufika kwa urahisi zaidi.

 

Dtk Lebba amesema katika utekelezaji wa zoezi la utoaji wa chanjo kwa watoto serikali ya mkoa wa Kigoma ilipokea zaidi ya shilingi milioni 70.5 kupitia ufadhili wa UNICEF huku wadau wengine wakiwa ni WHO.   

 

Amesema mafanikio yaliyojitokeza yametokana na ushirikiano wa wadau wengine wakiwemo   waandishi wa Habari , mashirika mbalimbali ikiwemo IRC ,CRS, THPS , MTI, RED CROSS, PATHIFINDER.

 

Akielezea chanzo cha kutoa chanjo hiyo kwa watoto chini ya umri wa miaka mitano amesema ni kutokana na taarifa za kuwepo kwa mlipuko wa ugonjwa wa polio katika eneo la Lilongwe nchini Malawi ambapo  amesema ugonjwa huo husambaa kwa kasi na kuadhiri zaidi watoto wadogo.

 

Ugonjwa huu unatokana na virusi na hauna tiba isipokuwa chanjo pekee na huambukizwa kupitia kinyesi na kushambulia mishipa ya fahamu na kusababisha mtoto kupooza”  

 

Hatua hivyo ya utoaji wa chanjo mbalimbali kwa watoto nchini Tanzania jamii imeelezwa kuwa na muamko mkubwa kwa asilimia 95 na hilo linatokana utekelezaji wa sera pamoja na  mpango Jumuishi wa Taifa wa malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto PJT-MMMAM ambao umekuwa ukizungumziwa sana na serikali katika kuelimisha jamii.

 

Ukiachilia mbali  mafanikioa hayo lakini pia Dkt. Lebba ameeleza baadhi ya changamoto zilizojitokeza wakati wa utekelezaji wa zoezi hilo kuwa ni pamoja na ufinyu wa bajeti, miundombinu kwa baadhi ya maeneo ni changamoto kuifikia kwa urahisi.

 

Baadhi ya wananchi akiwemo Joseph Kalyongwa ameeleza kutokana na elimu pamoja na hamasa inayotolewa na wataalamu wa afya kuhusu chanjo mbalimbali imesaidia jamii kuwa na uelewa wa kujitokeza kwa wingi kupata chanjo ili kulinda afya zao.

 

"Tuna imani kubwa na wataalamu wa afya kutika kulinda afya kinachohitajika ni elimu iendelee kuwafikia wananchi hususani wale waliopo vijijini hususani maeneo ambayo hayafikiki kiurahisi miundombinu yake bado si mizuri" alisema 

 

Kampeni ya chanjo hiyo ya Polio ilitekelezwa mkoani Kigoma kwa kipindi cha siku nne kuanzia Mei 12 hadi 15 ya mwaka 2022. 

Post a Comment

0 Comments