KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YAIPONGEZA TAWA

 

Makamu Mwenyekiti wa  Kamati ya Kudumu ya Bunge  ya Ardhi, Maliasili na Utalii Mhe. Shaban  Shekilindi (kulia) akizungumza mara baada ya Kamishna Uhifadhi wa TAWA, Mabula Misungwi kuwasilisha taarifa utekelezaji wa majukumu ya TAWA   kwa  Wajumbe wa Kamati hiyo ambapo ameipongeza TAWA kazi nzuri.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe.Balozi Dkt. Pindi Chana akizungumza leo Jijini Dodoma wakati wa kikao na Wajumbe wa  Kamati ya Kudumu ya Bunge  ya Ardhi, Maliasili na Utalii  wakati wa uwasilishaji wa utekelezaji wa majukumu ya TAWA

Kamishna Uhifadhi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) Mabula Misungwi akitoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja zilizokuwa zimeibuliwa na Wajumbe wa  Kamati ya Kudumu ya Bunge  ya Ardhi, Maliasili na Utalii  wakati wa uwasilishaji wa utekelezaji wa majukumu ya TAWA


Na Mwandishi Wetu, Dodoma.

Kamati ya Kudumu ya Bunge  ya Ardhi, Maliasili na Utalii imeipongeza Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) kwa  kuuza vitalu vya uwindaji vipatavyo 64 kwa njia ya mnada  wa kielektoniki kwa ufanisi ambapo uuzaji huu unaifanya TAWA ifikie asilimia 79 ya vitalu vyote vya uwindaji vilivyouzwa.

Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Shaban  Shekilindi (Mb) ametoa pongezi hizo  leo Oktoba 26, 2022 Jijini Dodoma   mara baada ya Kamishna Uhifadhi wa TAWA, Mabula Misungwi  kuwasilisha   taarifa utekelezaji wa majukumu ya TAWA   kwa  Wajumbe wa Kamati hiyo 

“Mimi pamoja na Wajumbe wa  kamati hii tunajisikia fahari sana kwa hatua hii ambayo TAWA mmeifikia kwani suala hili la kuanzishwa kwa mnada wa kielektoniki wa vitalu vya uwindaji wa kitalii lilikuwa na kelele nyingi kutoka ndani na nje ya nchi  '' amesisitiza Mwenyekiti huyo Shekilindi

Ameeleza kuwa mchakato wa kuanzisha mnada wa kielektoniki wa vitalu hivyo ulipigwa vita sana na baadhi ya Wafanyabiashara wakubwa waliokuwa wametawala katika biashara hiyo hivyo hawakutaka njia hiyo kwa hofu ya kupoteza vitalu walivyokuwa wamevimiliki kwa muda mrefu ila kutokana  na uongozi thabiti wa Wizara ya Maliasili na Utalii hawakurudi nyuma"

Kwa upande wake Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe.Balozi Dkt. Pindi Chana amesema zoezi hilo kwa kipindi  kirefu kabla ya kuanza kutumika kwa mfumo huo lilikuwa likikikumbwa na vitendo vya rushwa na ukiukwaji  wa kanuni na taratibu huku akibainisha kuwa matumizi ya mfumo wa kielektroniki yameifanya biashara hiyo itulie na sasa hakuna kashfa yoyote katika vitalu vilivyouzwa

''Kwenye mnada wa kiekektoniki, wafanyabishara wa vitalu vya uwindaji wanashindana kupitia mtandao tofauti na zamani ambapo wafanyabiashara walikuwa  wanakutana ana kwa ana na Watendaji wa Wizara'' amesema Balozi Dkt. Pindi Chana.

Ametumia fursa hiyo kuishukuru Kamati hiyo kwa uongozi madhubuti wa kulisimamia suala la  kuanzishwa kwa mfumo huo hali iliyopelekea Serikali kuongeza mapato.

Amefafanua kuwa kwa sasa hakuna kelele kwani Wafanyabiashara wa vitalu vya uwindaji wa kitalii wameanza kuelewa lengo la Serikali na kwamba hali hiyo ya mnada imesaidia kuwaibua wafanyabishara wadogo wanaoibukia katika biashara hiyo kwa kuwa minada hiyo imekuwa huru na inampa fursa mtu yeyote kushiriki.

Katika hatua nyingine Balozi Dkt. Pindi Chana amesema vitalu 24  bado havijauzwa akieleza kuwa hivi karibuni utatangazwa mnada mwingine kwa ajili ya vitalu vilivyobaki.

 

Post a Comment

0 Comments