Rais wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan na Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo wameshuhudia utiaji saini hati ya makubaliano (MOU) inayohusu ushirikiano katika masuala ya teknolojia (ICT), Posta na Mawasiliano baina ya nchi hizo.
Zoezi hilo lilifanyika, Ikulu Jijini Dar es Salaam hapo jana Oktoba23, 2022 ambapo kwa upande wa Tanzania, Mkataba huo umesainiwa na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhe. Nape Nnauye na kwa upande wa DRC umewekwa saini na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya nje wa DRC, Mhe. Christophe Lutundula.
Kwa mujibu wa taarifa ya Mkurugenzi wa mawasiliano ya Rais, Ikulu, Tanzania na DRC zimekubaliana kushirikiana na kuendeleza sekta ya mawasiliano kwa kuwa ni sekta pekee inayozalisha rasilimali pamoja na ajira kwa vijana kwa kiasi kikubwa.
Aidha katika kukuza jitihada za biashara kati ya nchi hizo mbili, Rais Samia alisema serikali ya Tanzania inaifanyia marekebisho meli ya MV Sangara ili ianze tena kutoa huduma ya kusafirisha mizigo kati ya Tanzania na DRC.
Aliongeza kuwa Tanzania na DRC kwa kushirikiana na Jumuia ya Afrika Mashariki (EAC) zina mpango wa kujenga ushoroba wa kati (Central Corridor) wa barabara itakayounganisha Tanzania na DRC.
Takwimu za biashara baina ya nchi hizo mbili zimepungua kwa
kipindi cha miaka 10 iliyopita, hivyo nchi hizo zimefufua Tume ya pamoja ya
Ushirikiano ili kukuza uhusiano na ushirikiano uliopo kwa manufaa ya nchi zote
mbili.
0 Comments