WANANCHI KASULU WAILALAMIKIA SERIKALI KUWAONDOA KATIKA MAENEO YAO



Na Emmanuel Matinde, Kasulu Kigoma

Wananchi wa Kaya takribani 400 katika Vijiji vya Kumtundu na Mvugwe katika Kata ya Nyamidaho Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma, wamelalamikia hatua ya serikali wilayani humo ya kuwaondoa katika maeneo waliyokuwa wakiishi na kufanya shughuli za kilimo na kupewa mwekezaji wa shamba la miwa na kiwanda cha sukari bila kuwalipa fidia yoyote.

Wakitoa malalamiko yao wananchi hao walisema mbali na kuondolewa pia mazao yao waliyokuwa wamelima yametaifishwa na nyumba zao kubomolewa ambapo wamesema wao hawapingi mwekezaji kuwekeza katika maeneo hayo, lakini hatua ya serikali kuwafurusha bila kuwalipa fidia ni kinyume na makubaliano yaliyofikiwa katika mkutano wa kuridhia maeneo yao yatumike kwa ajili ya uwekezaji.

Aidha katika upande mwingine wa mgogoro huo wananchi hao waliishutumu serikali ya wilaya ya Kasulu kwa kuchochea mgogoro baina ya wananchi baada ya kukata sehemu ya ardhi inayomilikiwa kihalali na baadhi ya wananchi wa kitongoji cha Mnarani eneo la Mkuyuni na kuwagawia wale walioondolewa katika eneo la uwekezaji.

Akizungumzia eneo linalolalamikiwa na wananchi hao lenye ukubwa wa hekta takribani elfu 38 Mkuu wa Wilaya ya Kasulu Kanali Isaac Mwakisu, alisema eneo hilo linamilikiwa kisheria na Kituo cha Uwekezaji Tanzania TIC ambalo walilipata kutoka kwa wananchi mnamo mwaka 2009.

 


Post a Comment

0 Comments