WATAALAMU WA MAABARA WATAKIWA KUJISAJILI KWENYE MFUMO NA KULIPA ADA KABLA YA JULAI 1,2023

Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Wataalamu wa maabara nchini wametakiwa kujisajili kwa njia ya mfumo kwani ifikapo Julai Mosi, 2023 ambao watakua hawajajisari hawatatambulika na baraza kama watoa huduma za maabara.

Hayo yamesemwa leo na Msajili Baraza la Wataalamu wa Maabara Nchini (HLPC) Bi. Mary Mtui wakati akitoa mafunzo ya miiko na maadili ya taaluma hiyo kwa wataalamu wa maabara katika Hospitali ya Benjamini Mkapa (BMH) Jijini Dodoma. 

"Kwa wale ambao wameshajisajili wanatakiwa kuhuisha usajili wao kwa kulipia ada ili kuepuka kutotambulika kimfumo na endapo utabainika unatoa huduma bila kutambulika sheria itachukua mkondo wake," amesema Bi. Mtui

Aidha, Bi. Mtui amesema ili kuboresha utoaji wa huduma za afya swala la miiko ya maadili na taaluma lazima lizingatiwe kwa watoa huduma za maabara nchini ili kuendana na kasi ya Serikali yetu chini ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan. 

"Kama wataalamu wetu hawana weledi, hawazingatii miiko, hawazingatii maadili basi huduma zitakazokuwa zinatolewa hazizingatii ubora unaotakiwa, hivyo tumekuja na mikakati ya kuangalia namna ya kuwafikia wataalamu wetu ili tuwape elimu hiyo," amesema Bi. Mtui

Hata hivyo, msajili Bi. Mtui amebainisha kuwa lengo la baraza hilo ni kuwafikia wataalamu wote wa Mkoa wa Dodoma kwa ngazi zote ili waweze kutoa elimu hiyo ya miiko na maadili kwa lengo la kuboresha huduma za afya nchini. 

"Pia, katika kusanyiko hili la leo tumeweza kupata mapendekezo kutoka kwa wataalamu hawa, tumeyachukua na kwenda kuyafanyia kazi kama baraza," amesema Bi. Mtui 

Katika kuelekea bima ya afya kwa wote Bi. Mtui amesema ni lazima tuhakikishe kwamba mtaalamu anaetoa huduma za maabara anakuwa na weledi kwa kuzingatia miiko na maadili ya taaluma. 

"Wataalamu wa maabara kote nchini tunatakia kujua kuwa weledi wetu, umahiri wetu na ubora wa huduma zetu ndio utakaofanikisha Serikali kupitia Wizara ya Afya kufikia malengo ya kuwezesha wananchi kujiunga na bima ya afya kwa wote," amesema Bi. Mtui

Post a Comment

0 Comments