WAKIMBIZI WA BURUNDI WAONGEZEWA MOTISHA YA FEDHA ILI WARUDI KWAO


Na. Deogratius Nsokolo,Kigoma
Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi UNHCR limeongeza motisha kwa wakimbizi wa Burundi wanaotaka kurejea nchini mwao kupitia mpango wa kuwarejesha kwa hiari unaoendelea.

Mkuu wa shirika hilo ofisi ya Kasulu Bw. Ben Diallo ameyasema hayo wakati wa uhamasishaji wakimbizi wa Burundi katika kambi ya Nyarugusu wilayani Kasulu Mkoani Kigoma na kuongeza kuwa ili kuongeza kasi ya wakimbizi kurejea kwa hiari mkutano wa pande tatu ambao umefanyika mapema mwezi huu mkoa wa Gitega nchini Burundi umeazimia kuongeza fedha kwa kila mkimbizi.

Amesema mkutano huo uliozihusisha nchi za Tanzania, Burundi na UNHCR umeongeza kiwango kutoka dola za kimarekani 75 kwa mtoto na dola 150 kwa mtu mzima na kufikia dola 200 kwa kila mkimbizi.

Makubaliano hayo yanakwenda sambamba na ongezeko la uzito wa mizigo inayobebwa na wakimbizi pamoja na Serikali ya Burundi kuweka mazingira wezeshi kwa wakimbizi wanaorudi ili waweze kupokelewa na kupewa maeneo ya kuishi sambamba na kujumuisha watoto katika elimu wanayosoma kwa sasa katika kambi za wakimbizi mkoani kigoma.

Diallo ameongeza kuwa kwa sasa maafisa kutoka mashirika yanayofanya kazi ya kuhudumia wakimbizi yatafanya kazi ya uhamasishaji kwa pamoja ili kuhakikisha wakimbizi wote wa nchi hiyo wanarudi Burundi.

Mkurugenzi wa Idara ya Huduma kwa Wakimbizi ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Bw. Sudi Mwakibasi akizungumza katika mkutano wa hadhara wa kuwahamasisha na kuwapa mrejesho wa mkutano huo kambini Nyarugusu amesema hatua hii ya motisha ni hatua ya pili katika utaratibu wa urejeshaji wakimbizi ikitanguliwa na urejeshaji wa hiari na sasa wanatoa motisha na hatua inayofuata ni ufungaji wa kambi.

Amesema mpango huo ni wa miezi sita ambapo wakimbizi zaidi ya elfu arobaini na tisa wanatarajiwa kuandikishwa kwa hiari na kurejeshwa kabla Serikali na UNHCR hawajafanya maamuzi mengine juu ya wakimbizi hao.

Ameongeza kuwa msingi wa makubaliano hayo ni kutokana na ukweli kwamba kwa sasa nchi ya Burundi iko na amani na wananchi zaidi ya milioni kumi na mbili wa nchi hiyo wanaendelea na shughuli zao hivyo hakuna sababu ya Tanzania kuendelea kuhifadhi wakimbizi.

"Katika mpango huu kila wiki wakimbizi 1400 watakuwa wakireshwa, nawaomba mchangamkie fursa hii muhimu ndani ya miezi sita hii hadi Novemba mwaka huu" alisema Mwakibasi

Nae Mratibu wa Kanda ya Magharibi wa Idara ya Huduma kwa Wakimbizi Bw. Nashon Makundi amesema kazi kubwa inayofanyika sasa ni uhamasishaji na utoaji elimu kwa wakimbizi na kwamba baadhi ya wakimbizi watapelekwa nchini Burundi kuona hali halisi ili waweze kuja na kuwaambia wenzao.

Ameongeza kuwaa tangu zoezi la kuwarejesha wakimbizi kwa hiari lianze mwaka 2017 zaidi ya wakimbizi 146,000 wamekwisharejeshwa na takriban wakimbizi 130,000 wamesalia katika kambi za Nyarugusu na Nduta.

Hata hivyo wakimbizi katika kambi ya Nyarugusu wametaka kuboreshwa zaidi kwa huduma na hasa fedha wanazopewa pamoja na kuhakikishiwa usalama wanapoamua kurudi kwao.

Mmmoja wa wakimbizi hao Ilambona John ametaka Jumuia ya Kimataifa kufikria pia kuwapeleka wakimbizi nchi za Ulaya kama wanavyopelekwa wakimbizi toka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Watu wa Kongo badala ya kufikiria kuwarudisha Burundi pekee.

 

Post a Comment

0 Comments