Mwajabu Hoza , Kigoma
HALMASHAURI ya Wilaya ya Kigoma Mkoani
Kigoma imepokea kiasi cha shilingi milioni 215.4 kwa ajili ya ujenzi wa
miundombinu ya madarasa ya elimu ya awali katika shule tatu kupitia mradi wa
Boost ambao umelenga kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia kwa
wanafunzi.
Elimu ya awali ndio
msingi wa elimu kwa wanafunzi wenye umri mdogo ambao wanaanza kuandikishwa
shule ambapo serikali imeona ipo haja ya kuboresha mazingira kwa kuanza
kutekeleza ujenzi wa madarasa na vyoo kwa ajili ya wanafunzi wa elimu ya awali.
Akizungumzia ujenzi
huo Kaimu Mkurugenzi Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma Egzavery Ntambara amesema
fedha hizo zitatumika katika ujenzi wa miundombinu ya madarasa mawili , matundu
ya vyoo mawili, madawati maalumu, mikeka pamoja na vifaa vya kuchezea.
“Ujenzi utafanyika
katika shule tatu na kila shule itakuwa na madarasa mawili bora na vyoo viwili
vya mfano ambapo gharama ya kila shule itakuwa ni shilingi milioni 71.8 ambayo
itakamilisha ujenzi na vifaa muhimu vyote kwa ajili ya wanafunzi wa elimu awali
kujifunzia” amesema.
Amesema wilaya hiyo
inajumla ya shule za msingi 109 ambapo kati ya hizo shule tatu ndio
zinatekeleza ujenzi wa madarasa ya awali ya mfano pamoja na matundu ya vyoo kwa
wanafunzi wa elimu ya awali.
Amesema mradi wa
Boost wa mwaka 2023 unatekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano na kila mwaka
ujenzi wa vyumba vya madarasa utakuwa ukifanyika kwa shule hizo za msingi na
kuhakikisha shule zote zinakuwa na madarasa ya awali.
Baadhi ya wananchi
akiwemo George Kasendeli na Emmanuel Bahindu wakazi wa kijiji cha Kabale
wanaishukuru serikali kwa kuwaletea mradi huo wa boost katika kijiji chao.
Wamesema watoto wao
kwa sasa wanasoma katika mazingira hatarishi ambapo kukamilika kwa madarasa
hayo kutasaidia kuondoa changamoto kwa wanafunzi ambao wanalazimika kutembea
umbali mrefu kufuata shule lakini pia msongamano mkubwa wa wanafunzi
katika darasa moja.
Agatha Rusimbi
anasema kwa sasa wanafunzi wanaoandikishwa shule wanakuwa na umri mdogo na
wanalazimika kupita maeneo ya vichakani kuelekea shule jambo ambalo ni hatari
sana kwa usalama wao hasa wale wa kike.
“Ujenzi wa shule
hii katika eneo letu utatupunguza hofu ambayo tunayo juu ya watoto wetu ambao
hadi sasa wanapita katika vichaka lakini pia changamoto za barabarani wakati
wakivuka kuelekea shule iliyopo kijiji cha jirani hivyo kukamilika kwa shule
hii itakuwa na manufaa makubwa sana kwetu na usalama wa watoto wetu utakuwa wa
kutosha” amesema Agatha
Diwani kata ya
Kalinzi Ignas Helanya anasema kata yake imepata ujenzi wa shule mbili za msingi
ambapo shule ya msingi Amani itajengwa katika kijiji cha Kabale na shule ya
msingi Bugugo ujenzi wake utakuwa katika kijiji cha Matyazo wilaya ya Kigoma.
Anasema ujenzi wa
shule hizo utasaidia kupunguza changamoto mbalimbali ikiwemo idadi kubwa ya
wanafunzi kwa baadhi ya shule pamoja na kuondoa changamoto ya utoro wa
wanafunzi ambao walikuwa wakitembea umbali mrefu kufuata shule.
Mkuu wa wilaya ya
Kigoma Salum Kalli amesema serikali imewekeza kwa kiasi kikubwa kwenye sekta ya
elimu katika ujenzi wa miundombinu ya majengo, matundu ya vyoo na madawati na
hivyo kupunguza mzigo mkubwa kwa wananchi ambao awali walilazimika kuchangia
ujenzi huo na ununuzi wa madawati.
“Kwa sasa elimu ni
bure kuanzia shule ya awali hadi kidato cha sita hivyo kazi yenu kubwa wananchi
wangu ni kuangalia mahitaji muhimu ya watoto ikiwemo sare za shule , madaftari
na kufuatilia kama anaenda shule, hakikisheni kunakuwa na mawasiliano
kati yenu na walimu kufuatilia maendeleo ya watoto shuleni” amesema
Serikali imeendelea
kuboresha sekta ya elimu kwa kuongeza fursa za ujifunzaji wa awali ambapo kwa
mwaka 2022/ 2023 kwenye mpango jumuishi wa Taifa wa makuzi, malezi na maendeleo
ya awali ya mtoto PJT – MMMAM zaidi ya shilingi bilioni 109 zimetengwa
kwa ajili ya uboreshaji huo.
0 Comments