MRADI WA BWAWA LA MWALIMU NYERERE KUONDOA TATIZO LA MGAO WA UMEME


Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Judith Kapinga, amesema kuwa majaribio ya mtambo na. 9 kwenye mradi wa kufua umeme wa Julius Nyerere wa Megawati 235 yamekamilika, na hivyo  utatua changamoto ya mgao wa umeme nchini.

Mhe. Kapinga ameyasema hayo  Februari 16, 2024, alipokuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Lupembe, Mhe. Edwin Sware aliyetaka kujua  miradi ya kimkakati ya umeme kama wa Julius Nyerere inaendeleaje na je ratiba ya majaribio imefikia wapi?

 Mhe. Kapinga alisema mradi huo unatekelezwa kwa weledi mkubwa na  mwezi Juni, mwaka huu ndio ilipaswa kuwashwa kwa mtambo no 9 , kutokana na jitihada za Serikali  unawashwa mwezi huu wa Februari.

"Nipende kulijulisha Bunge letu tukufu kuwa  hadi kufikia Jana tarehe 15 mwezi huu, majaribio ya mtambo huo namba 9 yalifanywa kwa kutembeza mashine hiyo hadi kwenye kiwango chake cha mwisho cha Megawati 235 na majaribio yamefanikiwa kwa kiasi kikibwa" Alisisitiza Mhe. Kapinga.

Aidha, Mhe. Kapinga alisema kwa sasa wataalamu wa mradi wa Julius Nyerere wako kwenye hatua za mwisho za kukamilisha majaribio ikiwemo kuweka ulinzi wa mtambo, ili kuingiza kwenye mpango wa kuzalisha umeme na kuongeza kuwa ratiba ya uzinduzi wa mradi iko pale pale mwezi wa pili mwaka huu.

Aidha Mhe. Kapinga amesema kuwa kwa upande wa mtambo na. 8  wa kuzalisha umeme utaanza kuzalisha mwezi Machi, 2024.

Kuhusu suala la mgao wa umeme Mhe. Kapinga amesema kuwa, hadi kufikia  mwezi wa tatu mwaka huu, mgao wa umeme utakuwa umeisha  kutokana na kuanza kwa mradi wa kuzalisha umeme ya Julius Nyerere.

Post a Comment

0 Comments